Header Ads

Header ADS

Wachimbaji Wadogo Wawili wa Madini Wamefariki Katika Mgodi uliopo Mkoani Mara



Wachimbaji wadogo wawili wa madini wamefariki dunia na kujeruhiliwa watu nane baada ya kuangukiwa na kifusi katika mgodi wa Irasaniro Buhemba mkoani Mara.

Waliofariki ni Kisambi Daudi (30) mkazi wa Magunga Wilaya ya Butiama na Marwa Mwita Magige (48) mkazi wa Nyaburundu wilaya ya Bunda ambao wamefariki usiku wa Juni 11, 2020.

Wamefariki baada ya kufukiwa na kifusi na kuokolewa wakiwa wamefariki na miili yao imehifadhiwa katika kituo cha afya Nyamuswa.

Waziri wa Madini, Dotto Biteko amesema, chanzo cha vifo hivyo ni kutokana na ukaidi wa wachimbaji wadogo kutofuata maelekezo ya wataalamu wa madini.

Amesema, eneo lilitokea vifo hivyo lilizuiliwa na Mkurugenzi wa Migodi nchini, Dkt. Abdruhamani Mwanga kutoka Tume ya Madini aliyetembelea eneo hilo siku chache zilizopita na kuzuia eneo hilo lisichimbwe kabla ya vifo hivyo kutokea.

Biteko ameongeza kuwa, pamoja na katazo hilo wachimbaji hao walikwenda usiku na kuanza kuchimba.

Ameongeza kuwa, endapo wachimbaji hao wasingekaidi maelekezo ya wataalamu madhara hayo yasingetokea.

Biteko amepiga marufuku uchimbaji wa madini wakati wa usiku na kuitaka ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Butiama na kamati ya ulinzi na usalama kuhakikisha uchimbaji wa usiku haufanyiki.


No comments

Powered by Blogger.