Header Ads

Header ADS

TBS yawatoa wasiwasi watumiaji marumaru



SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limewahakikishia Watanzania kwamba  limejidhatiti kuhakikisha linasimamia ipasavyo kiwango Na: 954 cha  mwaka 2008 ili marumaru (tiles) zinazozalishwa nchini na zinazotoka nje ya nchi zikidhi kiwango cha ubora kinachotakiwa.


Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Ofisa Viwango wa TBS Kitengo cha Uhandisi Ujenzi, Mhandisi Innocent Johnbosco, amesema viwango vya ujenzi wa marumaru vimegawanyika kupitia kiwango hicho kutengemea na uzalishaji na namna marumaru zinavyonyonya maji.


Amesema kiwango Na: 954 kimefafanua ubora wa uzalishaji wa marumaru zinazokidhi matakwa ya soko na kukidhi malengo yaliyokusudiwa.


Johnbosco amesema kuna marumaru za matumizi mbalimbali, ambapo zipo zinazotumika makanisani ambazo zinakanyangwa na watu wengi zaidi kuliko za majumbani na vyooni.


"Hapa nchini kuna viwanda viwili vya marumaru kupitia kiwango hiki, TBS tumekuwa tukidhibiti ubora wa marumaru zinazozalishwa hapa nchini na zile zinazotoka nje ya nchi.


Tumekuwa tukizifuatilia ipasavyo wakati wa uzalishaji wake,"amesema Mhandisi Johnbosco na kuongeza;


"Mwenendo wa soko kwa bidhaa za marumaru zinazozalishwa nchini ni mzuri hadi kufikia kuuza nje ya nchi kutokana na marumaru zinazozalishwa kuendana na viwango."


Aidha, alisema watumiaji wanatakiwa kuhakikisha kabla ya kununua marumaru hizo kujiridhisha na viwango vilivyowekwa nje ya vifungashio na kuangalia ni aina gani ya marumaru wanazohitaji kuweka sehemu wanazotaka kuwekwa.


"Madhara yaliyopo katika marumaru ambazo zipo chini ya kiwango ni pamoja na kupasuka nyayo za miguu, kupasuka kwa marumaru zenyewe na kuanguka baada ya kutengenezwa,"amesema




No comments

Powered by Blogger.