Header Ads

Header ADS

Mkuu wa Polisi wa Atlanta nchini Marekani Ajiuzulu Baada ya mtu Mweusi Kuuawa



Mkuu wa polisi wa Atlanta nchini Marekani amejiuzulu baada ya mwanaume mweusi aliyekuwa amelala kwenye gari lake kupigwa risasi nje ya mgahawa mmoja.

Rayshard Brooks, 27, alipigwa risasi Ijumaa jioni, mamlaka imesema.

Mayor Keisha Lance Bottoms amesema Erika Shields amejiuzulu Jumamosi.

Waandamanaji huko Atlanta waliandamana barabara wikendi hii wakitoa wito wa hatua kuchukuliwa kufuatia kifo cha Bwana Brooks'.

Mgahawa wa Wendy ambao mwanaume huyo ameuawa pia umechomwa moto.

Katika kipindi cha wiki tatu, watu kote Marekani wamekuwa wakiandamana kufuatia kifo cha George Flyod, mwanaume mweusi aliyekufa mikononi mwa polisi.

Erika Shields amehudumu kama mkuu wa polisi tangu Desemba 2016 na kufanyakazi katika idara ya polisi ya Atlanta kwa zaidi ya miaka 20. Ataendelea kuwa katika idara hiyo lakini atatekeleza majukumu mengine, Meya Bottoms amesema.

''Kwasababu ya kutamani kwake Atlanta kuwa mfano wa mabadiliko yanavyotakiwa kuwa katika nchi hii, Shields ameamua kujiuzulu nafasi ya ukuu wa polisi ili mji huo usonge mbele katika kuujenga upya uaminifu wa polisi kwa jamii nzima,'' Meya alieleza kwenye taarifa yake.

Mmoja wa maafisa wa polisi waliohusika kwenye shambulio, Garrett Rolfe, amefukuzwa kazi na mwingine, Devin Brosan, amebadilishiwa majukumu. Wote wawili wamelitumikia jeshi la polisi kwa miaka sita, na miaka miwili kwa jeshi la polisi jijini Atlanta.

Kilichotokea Usiku wa Ijumaa

Idara ya uchunguzi ya Georgia inachunguza kifo cha Bwana Brooks na inatafuta video za kamera za usalama ndani ya mgahawa wa Wendy's na pia picha za mashuhuda.

Katika video ya mashuda, Bwana Brooks alionekana akiwa kalala sakafuni nje ya mgahawa wa Wendy's, akipambana na polisi wawili.

Aliikamata silaha ya polisi na kufanikiwa kukimbia. Afisa mwingine aliweza kutumia silaha ya umeme kumnasa Brooks, kisha polisi hao wawili walitoweka kwenye video hiyo.

Milio ya risasi kisha ikasikika na bwana Brooks alionekana akiwa amelala chini.

Alipelekwa hospitali lakini baadae alipoteza maisha. Mmoja wa polisi alitibiwa majeraha aliyoyapata kwenye tukio hilo.

Ofisi ya mwanasheria wa kaunti ya Fulton inafanya uchunguzi wake kuhusu tukio hilo, imesema katika taarifa yake.

Je,Trump yuko mashakani kwa msimamo wake kuhusu ubaguzi wa rangi?

Video za kughushi za maandamano Marekani

Mawakili wanaowakilisha familia ya Brooks imesema afisa wa polisi hakuwa na haki ya kutumia nguvu kupita kiasi, akisema silaha aliyokuwa amekwapua bwana Brooks haikuwa silaha hatarishi.

''Huwezi kumfyatulia mtu risasi isipokuwa kama amekuelekezea silaha,'' Mwandesha mashtaka Chris Stewart alisema.

Waandamanaji walikusanyika nje ya mgahawa wa Wendy's siku ya Ijumaa, kwa mujibu wa New York Times.

Maandamano yalianza tena katikati ya mji wa Atlanta siku ya Jumamosi. Picha za maandamano zikiwa zimeandikwa jina la Brookes na Black Lives Matter zilionekana zikiwa zimebebwa na waandamanaji.

Watu mjini Atlanta tayari wamekuwa kwenye maandamano baada ya kifo cha George Floyd. Aliyekufa tarehe 25 mwezi Mei baada ya polisi wa Minneapolis kumkaba kwa goti lake kwa zaidi ya dakika nane. Afisa huyo amefukuzwa kazi na kushtakiwa kwa mauaji.

No comments

Powered by Blogger.