Header Ads

Header ADS

CHINA: Marekani Haitofika Popote kwa Kutumia vibaya Azimio Nambari 2231



Chen Xu, Mwakilishi wa China katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, mapatano ya JCPOA ni mapatano ya pande kadhaa na kusisitiza kuwa, juhudi za kutumia vibaya azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, hazitofikia popote.

Mwakilishi huyo wa China katika Umoja wa Mataifa ameyasema hayo kupitia ujumbe alioutuma kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter na kubainisha kwamba mapatano ya JCPOA yalikuwa ya pande kadhaa ambayo yalipata uungaji mkono wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na kwa mtazamo wa kisheria ni lazima yatekelezwe. Aidha Xu amezitaka pande zote husika za mapatano hayo kutekeleza ahadi zao ndani ya JCPOA. Sambamba na kukaribia muda wa kufutwa vikwazo vya silaha vya Umoja wa Mataifa dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, ambavyo pia ni sehemu ya azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama la UN, Wamarekani wanafanya njama kubwa kujaribu kuzuia kuhitimishwa vikwazo hivyo.

Hivi karibunii, serikali ya Marekani ilisambaza utangulizi wa azimio kwa wanachama wa baraza hilo ikiwataka warefushe muda wa vikwazo vya silaha vya umoja huo dhidi ya Iran. Pamoja na hayo upitishwaji wa azimio hilo unategemea kuungwa mkono na wanachama 9 wa Baraza la Usalama tena bila kupigiwa kura ya veto na China na Russia.  Pamoja na kwamba Marekani kwa miaka miwili iliyopita na bila kuzingatia azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama, ilijiondoa katika mapatano ya nyuklia ya JCPOA, inadai katika tafsiri yake mpya kwamba kwa mujibu wa azimio hilo bado ni mmoja wa wanachama wenye taathira katika JCPOA.

No comments

Powered by Blogger.